ECKROS SCHOOL OF JOURNALISM

eckroscollege. Powered by Blogger.

Blogroll

About

Habari za Mahusiano Kila siku

JOURNALISM STUDENTS AT ETC COLLEGE

JOURNALISM STUDENTS AT ETC COLLEGE

ETC RADIO ONLINE LIVE

http://wwweckrosnewsblogspo.radio12345.com/

TUMEDHAMIRIA KUWATUMIKIA WATANZANIA - MAJALIWA

Sunday, November 29, 2015

     
WAZIRI MKUU Majaliwa Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuhakikisha kila kinachokusanywa kama mapato ya nchi kinatumika kwa maslahi ya Watanzania wote na si kwa manufaa ya wachache.

Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumapili, Novemba 29, 2015) wakati akifunga maadhimisho ya miaka 20 ya Dayosisi ya Pwani ya Kanisa la African Inland Church Tanzania (AICT) kwenye ukumbi wa PTA, viwanja vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

“Serikali imeanza kukabiliana na upotevu wa mapato ya Serikali na kuepuka matumizi yasiyo ya lazima ya fedha za umma. Nia yetu ni kuhakikisha kila kinachopaswa kukusanywa kama mapato ya nchi, kikusanywe na kitumike kwa masuala ya msingi kwa ustawi wa Watanzania wote na si kwa watu wachache,” alisema.

Akifunga maadhimisho hayo kwa niaba ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Waziri Mkuu alisema Serikali imedhamiria kupambana na maovu yote na kuondoa kero zinazowaumiza wananchi wa kawaida. “Wako watu wanaoamini kwamba hatuwezi, nawaomba waondoe hiyo dhana. Wako watu wanaodhani kwamba kwamba utawala huu ni wa watu wapole, nao pia waondoe hiyo dhana,” alisema huku akishangiliwa na mamia ya waumini waliohudhuria sherehe hizo zilizoanza Novemba 27, 2015.

“Tunawaomba Watanzania wote mtuunge mkono kwenye vita hii na mtuwezeshe kuifanya kazi hiyo. Tunaomba waumini wote mtuombee katika sala zenu za kila siku ili tuweze kuongoza kwa haki na kuwaletea Watanzania wote maendeleo,” aliongeza.

Akinukuu kitabu cha Mithali sura ya 29 mstari wa pili, Waziri Mkuu alisema: “Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi, bali mwovu atawalapo, watu huugua. Mtuombee viongozi wenu tuwe waadilifu na wenye kutenda haki. Nasi tutaendelea kuwa waadilifu ili watu wetu wasigue,” alisema.

Aliwataka viongozi wa kanisa hilo waendelee kuisaidia Serikali katika kujenga kundi la watu wenye maadili mema ili walisaidie Taifa kuwa na watu waadilifu na hivyo kupunguza kero nyingi zinazoikabili jamii.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na waumini wa kanisa la hilo kutoka mikoa mbalimbali, Askofu Mkuu wa Kanisa la AICT, Askofu Silas Kezakubi alisema Kanisa hilo litaendelea kumuombea Rais Dkt Magufuli na viongozi wenzake ili wawe na afya njema, wawe na hekima na kuahidi kwamba wataendelea kuwaweka chini ya ulinzi wa Mungu siku zote.

Alisema wao kama kanisa wanaamini kwamba Serikali ya awamu ya tano ina nia ya kuwatumikia wananchi kwa bidii na uadilifu lakini akasisitiza kuwa siri ya bidii na uadilifu inapatikana kwenye neno la Mungu.

Akisoma risala ya kanisa hilo, Askofu wa AICT Dayosisi ya Kibaha, Askofu Charles Salalah alisema kanisa halina budi kushirikiana na Serikali kwa sababu wote wanawahudumia watu walewale isipokuwa katika malengo tofauti.

Alisema kanisa hilo linahubiri maadili mema na bidii katika kazi kwa vile linaamini kuwa maendeleo hayadondoki kutoka juu wala hayaoti kama uyoga bali yanapatikana kwa watu kufanya kazi.

Akisisitiza kuhusu uadilifu, aliwataka wazazi kudumisha ndoa zao ili watoto wapate malezi mema kutoka kwa baba na mama na kwamba baba na mama wasipokaa vizuri, watoto hawawezi kuwa waadilifu.

“Wazazi tunao wajibu wa kupanda mbegu bora ya uzalendo kwa watoto wetu. Endapo tutapanda mbegu mbaya ya kuwagawa watoto wetu kwa itikadi tofauti, ni lazima tujue kuwa tutavuna tunachopanda.”

“Tukumbuke kuwa tunalo Taifa moja tu la Tanzania. Hata kama watoto wetu watakuwa na upenzi na vyama vyao, ni lazima tuwalee katika misingi ili wakue wakijua Taifa letu ni moja tu. Ndiyo maana tunaweka mkazo kwenye familia kwa sababu maadili mema yanaanzia nyumbani,” alisisitiza.                                                                                                          

BREAKING NEWZZZZ. KATIKA KUPUNGUZA MATUMIZI YA SERIKALI, KUTHIBITI UCHAPISHAJI OFISI ZOTE ZA UMMA


ECKROS SCHOOL OF JOURNALISM NJOMBE KUFANYA MAHAFALI YA TATU

Chuo cha habari njombe kinatarajia kufanya mahafali yake ya tatu hapo jumamosi tarehe tano katika ukumbi wa chuo cha maendeleo. Sherehe zinatarajiwa kuanza saa tano asubuhi kwa maandamano toka chuoni ndani ya uwanja wa sabasaba na kuelekea ukumbini.

Nyote munakaribishwa.
Imetolewa na uongozi

MAJIPU MATANO SUGU KWA RAIS DK. MAGUFULI,AKIWEZA KUYATUMBUA HAYA ATAKUWA AMEKATA KIU YA WATANZANIA

Saturday, November 28, 2015

Wasomi, wanasiasa na watu kutoka makundi mengine ya jamii wamesema Rais John Magufuli atapimwa katika miaka mitano ijayo kwa mambo makubwa matano yaliyoonekana kuwa ‘majipu sugu’ na changamoto kwa mtangulizi wake, Jakaya Kikwete.
Majipu (mambo matano) hayo ni kudhibiti mtandao wa wafanyabiashara wa dawa za kulevya, kukomesha rushwa na ufisadi, kufumua mtandao wa majangili, kuhakikisha Katiba Mpya inapatikana na kuua ‘mchwa’ unaoitafuna fedha za Serikali.
Maoni yaliyotolewa na wasomi, wanasiasa na wananchi wa kawaida yanaonyesha kwamba kufanikiwa kwake kutategemea aina ya ushirikiano atakaoupata kutoka kwa wananchi na wanasiasa na hasa wa kutoka chama chake.
Mhadhiri kutoka Idara ya Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Elijah Kondi alisema Dk Magufuli anahitaji kupigana vita kali kufanikisha ahadi zake na akaonya kuwa hawezi kusimama mwenyewe na kushinda vita hiyo bila kuungwa mkono na wananchi hasa chama chake, CCM.
“Vigogo wengi ndani ya chama chake wamekuwa wakihusishwa na majipu hayo. Hivyo, kufanikisha azma hiyo, kutategemea wingi wa wanaCCM watakaomuunga mkono, lakini kama watakuwa wachache, itakuwa vigumu. Hilo hata yeye (Magufuli) analifahamu ndiyo maana anasema vita hiyo ni kubwa,” alisema Kondi.
Pia, alisema kushughulikia mtandao wa dawa za kulevya, ujangili na kuanzisha mahakama ya mafisadi kutategemea ushirikiano atakaoupata kutoka kwa watendaji na baraza lake la mawaziri.
Kondi alisema kushindwa kwa Rais mstaafu Kikwete katika mambo hayo kulitokana na udhaifu wa baraza lake la mawaziri na watendaji wa taasisi za Serikali. “Rais anaweza kuwa na dhamira njema, lakini je, atapata mawaziri wazuri wa kumsaidia? Hao mawaziri watakuwa na ari gani ya kushiriki vita hiyo?” alihoji na kuongeza:
“Kwa sababu anaweza kuanzisha mahakama ya mafisadi lakini ikashindwa kuonyesha uhai kama anavyotarajia. Jaribio la kutumbua majipu hayo itategemea ushirikiano wa chama chake, mawaziri atakaowateua na watendaji wa Serikali.”
Mhadhiri wa Idara ya Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Richard Mbunda alisema kilichosababisha marais waliomtangulia kushindwa kutumbua majipu hayo ni utofauti mkubwa ulioonekana kati yao.
“Utofauti katika uwezo wao ukoje? Dhamira zao zinatofautianaje? Lakini hata kiwango cha utashi wa kushughulikia hilo jipu kinatofautianaje na uongozi uliopita. Ukisikiliza kauli ya Rais Magufuli anaonyesha matumaini,” alisema Mbunda.
Meneja wa Soko la Machinga Complex, Nyamsukura Masondore alisema kupandishwa mahakamani kwa vigogo wa Serikali katika kashfa ya EPA ni sehemu ya juhudi zilizoonekana kwa uongozi uliopita. “Hivyo, hakuna kitakachoshindikana kwa Rais Magufuli endapo watendaji wa chini watakuwa tayari kubadilika na kutoa ushirikiano wa kushinda vita ya majipu hayo,” anasema
Profesa George Shumbusho wa Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema ana imani Rais Magufuli anaweza kushughulikia changamoto hizo sugu ambazo ameziita majipu kutokana na historia ya utendaji wake. “Rais Magufuli atafanikiwa kazi hiyo kutokana na historia yake ya kutojihusisha kwa karibu na mtandao wa wafanyabiashara wakubwa hapa nchini na nje,” alisema.
Profesa Shumbusho alisema kuwa endapo ataendelea na msimamo huo, changamoto ya ukwepaji kodi, misamaha ya kodi, biashara haramu ikiwamo ya dawa za kulevya zitakoma.
Dawa za kulevya
Aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alinukuliwa Agosti 2013 bungeni akikiri kuwapo baadhi ya majina ya wabunge miongoni mwa watu wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya lakini alisema Serikali haiwezi kuwataja hadharani kwa haraka.
Hata Kikwete wakati wa awamu yake ya kwanza, aliwahi kusema anawajua wauza dawa za kulevya lakini tatizo hilo limeendelea kuwa sugu hadi anamaliza kipindi chake cha pili.
Mwaka huohuo, Umoja wa Mataifa (UN) ulitoa ripoti inayobainisha Tanzania kuwa kinara wa kupitisha dawa za kulevya katika nchi za Afrika Mashariki. Kuanzia 2010 hadi 2013 ilipitisha tani 64 za dawa za kulevya aina ya heroine na ikitaja Bandari ya Tanga kuwa njia kuu ya upitishaji huo.
Je, baada ya kuanzishwa kwa Sheria ya Kupambana na Kuthibiti Dawa za Kulevya ya mwaka 2015, Rais Magufuli ataweza kusimamia mapambano dhidi ya vinara wa biashara hiyo?
Ujangili wa tembo
Kabla ya kuondoka madarakani, Rais Kikwete aliwahi kunukuliwa Februari 2014 na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC Swahili) akikiri kuwatambua majangili 40 wa meno ya tembo na kwamba kiongozi wao anaishi Arusha. Pia, alikiri kuwa vita dhidi ya ujangili ni tatizo sugu.
Vilevile, Mei 2014, ripoti iliyoitwa ‘Ivory’s Curse: The Militarization and Professionalization of Poaching in Africa’, ilieleza kuwa tangu mwaka 2000 wizara inayohusika na utalii ilikuwa imetawaliwa na kashfa za rushwa. Ripoti hiyo ilifafanua jinsi vikundi mbalimbali vya waasi barani Afrika vinavyoendesha shughuli za ujangili.
Katiba ya Jaji Warioba
Oktoba 2014, Bunge Maalumu la Katiba lilipitisha Katiba Inayopendekezwa kwa tofauti ya kura mbili tu zilizonusuru kukwamisha Katiba hiyo kwa upande wa Zanzibar. Mvutano kati ya CCM na upinzani wakati wa upitishaji wa Katiba hiyo ulitokana na tofauti za itikadi na sera kuhusu muundo wa Muungano.
Wajumbe wa CCM walipigania sera yao ya muungano wa Serikali mbili wakati wenzao wa wapinzani walipigania muundo uliopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji mstaafu, Joseph Warioba wa Serikali Tatu. Hadi sasa haijapigiwa kura ya maoni.
‘Mchwa’ Serikalini
Kila mwaka, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) amekuwa akikagua na kuibua ufisadi mkubwa katika Serikali Kuu, Idara za Serikali na mashirika ya umma. Ripoti iliyotolewa mwaka huu inaonyesha ukaguzi ulifanyika katika taasisi 176 za Serikali kuu, halmashauri 163 na mashirika ya umma 109. Kikwete amewahi kupangua baraza lake la mawaziri na kuwafukuza kazi watendaji lakini bado ufisadi umeendelea katika nyanja tofauti kama ulipaji mishahara hewa na ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo.
Mahakama ya mafisadi
Moja ya ahadi kubwa za Rais Magufuli wakati wa kampeni na Novemba 20 alipozindua Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano ni kuanzisha Mahakama Maalumu ya kushughulikia mafisadi. Tayari mchakato umeanza lakini wachambuzi wanasema kinachotakiwa ni kuipa meno Taasisi ya Kudhibiti na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ili iweze kufanya kazi zake bila kuogopa mtu.

MO APATA TUZO NYINGINE, ADHIHIRISHA TAMAA YA KUWATUMIKIA WATANZANIA

Mfanyabiashara maarufu ambaye pia ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Makampuni ya MeTL Group, Mohammed Dewji akitembea kwenye 'Red Carpet' mara baada ya kuwasili katika hotel ya Hilton Sandton jijini Johannesburg, Afrika Kusini kwenye hafla ya utoaji tuzo iliyoandaliwa na jarida maarufu la Forbes na kutunukiwa tuzo ya "Forbes Africa Person Of the Year 2015".(Picha zote na Zainul Mzige wa Modewjiblog).

Na Modewjiblog team
MFANYABIASHARA na mtu mwenye taasisi ya kusaidia jamii, Mohammed Dewji maarufu kama Mo ametunukiwa tuzo ya jarida maarufu la Forbes ya "Forbes Africa Person Of the Year 2015" katika hafla iliyofanyika Novemba 27 mwaka huu jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
Mfanyabiashara huyo pia ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Makampuni ya Mohammed Enterprises T Ltd (MeTL Group) kampuni iliyoanzishwa na na baba yake katika miaka ya 1970 ambayo sasa imekua na kujikita katika viwanda vya nguo, usagaji nafaka, utengenezaji wa vinywaji baridi, usindikaji wa mafuta ya kula, usindikaji wa chai na kuendesha mashamba ya mkonge ambapo tayari anashea ya asilimia 40 ya soko.
Mo ametwaa tuzo hiyo kwa kuwashinda watu watano mashuhuri barani Afrika. Watu hao ni Nkosazana Dlamini Zuma, mke wa Kwanza wa Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma. Mama huyo kwa sasa ndiye Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU). Mwingine ni Rais wa sasa wa Nigeria, Muhammadu Buhari aliyetambuliwa kutokana na kuanzisha vita dhidi ya rushwa nchini mwake.
Aidha wapo Arumna Otei, mchumi mahiri raia wa Nigeria ambaye kwa sasa ni Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia. Pia alikuwemo Mwandishi maarufu wa vitabu wa Nigeria, Chimanda Ngozi Adichie ambaye moja ya vitabu vyake vinaelezea picha halisi ya Afrika inavyofikiriwa duniani.
Akitoa neno la shukurani baada ya kukabidhiwa kwa tuzo hiyo Mo, alisema anatoa tuzo hiyo kwa vijana wa Kitanzania kwani ndio nguvu kazi inayobeba uchumi wa nchi.
Mo ambaye kampuni yake ya MeTL inaongoza kwa kutoa ajira nchini, ikiwa imetoa ajira 26,000 kote katika viwanda vyake 31 vilivyopo nchini na katika mataifa matano ya Afrika, alisema amefurahishwa na tuzo hiyo ambayo anaitoa kwa vijana kwa kutambua pia wajibu mkubwa walionao katika kukabiliana na umaskini.
Alisema ajira 26,000 zimegusa watu wengi nchini na kwamba ana matumaini makubwa ya siku za usoni kutoa ajira zaidi kutokana na biashara zake kuendelea kukua.
"Heshima yangu kubwa haitokani na utajiri, maana kama utajiri wako hauna msaada wala kugusa watu masikini hauna maana yeyote, hivyo basi heshima hii ni kutokana na kwanza bidhaa zangu kugusa maisha ya watu kila siku kuanzia sukari na majani ya chai asubuhi pamoja na unga wa ngano, lakini pia chakula cha mchana kwa unga wa sembe, mafuta ya kupikia na maji ya kunywa, bidhaa zote hizo za Mohammed Enterprises zinagusa maisha kila nyakati katika siku.
"Nina viwanda 31 ambavyo vimekuwa vikitengeneza bidhaa za Kitanzania na kuziuza kwa Watanzania kwa bei yenye unafuu mkubwa, mathalani tunauza maji kwa bei chini ya dola moja kwa shilingi za Kitanzania 200, hakuna hata Ulaya, nina kiwanda cha khanga na vitenge ambacho malighafi zake zote ni za Kitanzania, hivyo kuna kusaidia serikali kwa kulipa kodi ipasavyo, lakini pia kusaidia moja kwa moja ajira za Watanzania walio wengi ambao tatizo lao kubwa katika kundi la vijana ni ajira"
Alitumia fursa hiyo kumshukuru na kumpongeza baba yake kwa kumwita mjasiriamali shujaa ambaye alitoka kuanzia dereva wa malori baada ya kuhitimu kidato cha nne mwishoni mwa miaka ya 1960 hadi kufikia ubilionea. Alisema alipata maono ya utajiri hasa kutoka kwa baba yake huyo aliyekuwa akimshirikisha biashara tangu akiwa mdogo.
“Mwanaume mwenye ndoto huhitaji mwanamke mwenye maono. Na nimebarikiwa mwanamke ambaye kwa miaka 15 amekuwa akinipa sapoti isiyoyumba.
“Saira, nina shukurani nyingi kwako kwa kuwa nguzo ya familia yetu, mama wa heshima kwa watoto wetu watatu,” alisema Mo kwenye hafla hiyo.
Kwa utulivu, Mo alisema: “Baba, zawadi kubwa ambayo ulinipa katika maisha yangu ni muda wako, na kwa hilo nitakuwa mwenye deni la shukurani kwako siku zote za maisha yangu.”
Mo ambaye moyo wake wa binadamu ulimfanya awanie uwakilishi Jimbo la Singida Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kushinda nafasi hiyo na hivyo kuwawakilisha wanasingida kuanzia 2005 na 2015 amesema maisha ni changamoto kubwa inayobadilishwa kwa utumishi wenye nia ya dhati kwa umma.
Alisema alipowania uwakilishi alikuwa na sababu: “Nilikuwa na umri wa miaka 24, nilikwenda Singida kutoa heshima kwenye kaburi la marehemu babu yangu. Sikuwa nimefika huko tangu nilipoondoka nikiwa na umri wa miaka mitatu.
“Nilipokuwa njiani, nilimuona mzee akiwa na maji yenye rangi ya njano, machafu ambayo aliyatumia kwa kunywa. Nilishangaa, maana hali ile sikuwahi kufikiri kama ipo vile. Kipindi hicho nilikuwa nimemaliza Chuo Kikuu cha Georgetown, Marekani.”
Mo anasema kuwa aliingiwa na hisia kutaka kujua nini hasa alichokuwa anahitajika kufanya, alimfuata yule mzee aliyekuwa na maji yale, alipozungumza naye, aliwazungukia watu wengine na kuridhika kuwa ile ndiyo hali halisi, hapo ndipo fikra ya kwa nini agombee ubunge ilipoanzia.
Anasema kuwa baada ya kujiridhisha hivyo, alirudi kwa mzee wa kwanza, alizungumza naye na kumuuliza ni kwa nini shida ile ilikuwa haizungumzwi kwa upana katika mamlaka husika.
“Nilipojitambulisha yule mzee alisema anamkumbuka babu yangu, kisha akanishauri nigombee ubunge, alinisisitiza mno ili nisaidie kuondoa lile tatizo la watu wa Singida kunywa maji machafu,” alisema Mo.
Anaeleza kuwa alipokuwa njiani kurejea Dar es Salaam, alilifikiria tatizo hilo kwa mapana zaidi, akalifanyia utafiti na kubaini kwamba katika kila watu 10, watatu walikuwa wakipoteza maisha kutokana na maradhi yanayosababishwa na maji machafu.
Anaendelea kusema kuwa aligundua kuwa Singida kulikuwa na tatizo kali la maji safi na salama. Anasema kuwa alibaini uwepo wa tatizo la elimu kuhusu matatizo ya maji.
Jambo lingine ambalo anasema aliligundua ni uwepo wa tatizo la huduma za afya. “Niliwafikiria watoto wangu, jinsi ninavyowapenda, na namna ambavyo kila mzazi anavyompenda mwanaye. Nilipingana na hali kuwa watoto wa Uingereza na Marekani wamependelewa zaidi. Maisha ni sawa bila kujali chochote,” anasema Mo.

MAKUNDI YA JAMII ASILIA YA WAHADZABE, WABARABAIG, WAMASAI WAIOMBA SERIKALI YA TANZANIA KUWATAMBUA KAMA JAMII NYINGINE

Friday, November 27, 2015

Na Andrew Chale, Modewjiblog

Jamii ya watu wa asili na makundi yao wameiomba Serikali ya Tanzania kutambua uwepo wao hapa nchini ikiwemo kuwatangaza kwa mema na kuwasaidia kwa misingi ya haki, hutu na kimaendeleo kama watu wengine wanaotambulika ndani na nje ya mipaka yao.

Hayo yameelezwa mapema leo jijini hapa wakati wa uzinduzi wa taarifa ya Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kuhusu utafiti wa Hali ya Haki za watu wenye kuishi maisha asilia Tanzania wakiwemo makabila ya Wa-Akiye,Wa- Hadzabe,Wa- IIparakuyio Masai na wengine wengi.

Akielezea katika uzinduzi huo mmoja wa wajumbe walioandaa taarifa ya Tume hiyo, ambaye anatoka nchini Kenya, katika taasisi ya African Commission on Human and Peoples Rights (ACHPR), Dk. Naomi Kipuri amebainisha kuwa jamii ya watu asilia wamekuwa na kilio cha muda mrefu cha kutaka kupata haki zao zao msingi na kutambulika zaidi.

“Utafiti tuliofanya jamii ya watu asilia wamekuwa katika malalamiko ya muda mrefu ikiwemo kutaka haki zao za msingi. Ikiwemo masuala ya elimu, makazi na haki zingine. Pia wameomba Serikali kuwatangaza watu hawa wa asilia ili wasionekane wageni kwani jamii nyingi bado hazijawatambua na hata kupelekea kuwavunjia hutu wao” alieleza Dk. Naomi.


Aidha, Dk. Naomi katika uwakilishi wake wa mada kwenye mkutano huo amelezea namna ya jamii inavyoendelea kuwaona watu hao ni tofauti kiasi cha kupelekea watu hao kudumaa na maisha yale yale ya asilia.
“Jamii zingine zinawatenga watu wa jamii ya Wamasai, tumeshuhudia lugha na matamshi kwenye mizunguko ya watu ikiwemo kwenye madaladala, mitaani huku wakimuona Mmasai kama mtu tofauti, sasa katika ripoti hii imeweza kuelezea mambo mengi sana. Ikiwemo suala la Haki ya kuishi, kufanya kazi na mambo yote kama watu wengine” alimalizia Dk. Naomi. 

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu, Mh. Idd Ramadhan Mapuri ameeleza kuwa kupitia ofisi yake itahakikisha inashughulikia suala hilo la kuwa karibu na watu asilia na kutambua misingi ya haki zao ambapo amebainisha watu hao wa asilia kwa Tanzania wanafikia makundi zaidi ya sita. 

Kwa upande wao baadhi ya wawakilishi wa watu hao wa watu asilia wakielezea katika mkutano huo, waliomba na wao na wapate wawakilishi maalum ikiwemo Bungeni ama sehemu za maamuzi ikiwemo Halmashauri na maeneo mengine ya Serikali ilikutambua michakato ya Kimaendeleo kwa kina. “Jambo la ardhi, ndilo linalotuumiza kwa sasa.

 Sie tunaporwa ardhi yetu kila siku na kesi nyingi ni za kuporwa ardhi na migogoro ya wakulima na wafugaji, ndani ya migogoro hii ina siri kubwa bila kujua kiini chake ni wakati wa kufika kule na kupata ukweli zaidi” alielezea Adam Ole Mwarabu Kwa upande wake, Mratibu wa NGONET Ngorongoro, Samweli Nangiria ambaye anawakilisha watu hao asilia anaeleza kuwa, wao wamekuwa wakitambuana kwa desturi ikiwemo suala la ufugaji na maisha mengine, Jamii nyingine imekuwa wakiwaona wao ni watu wa tofauti kiasi cha kupora mali zao ikiwemo ardhi, mifugo na mambo mengine ya msingi. 
“Sie watu asilia tuna mahusiano mbalimbali na jamii zetu za kifugaji licha ya jamii zingine kutuingilia kwenye maeneo yetu na kupora ardhi yetu. Watu asilia tunahitajika kutambulika zaidi na hata kupatiwa huduma muhimu ikiwemo kujengewa shule, vyuo na mahitaji mengine ikiwemo haki na hutu kama watu wengine.” Alieleza Samweli Nangiria.

Kwa upande wake, .. ameweza kuipongeza tume ya Haki za Binadamu kwa kuweza kushughulikia suala hilo na hata kuandaa tukio hilo kwa kushirikisha wadau wengine wakiemo wao wa asilia.

“Tanzania ndio nchi ya kwanza kuaandaa kikao cha Afrika kwa watu hawa wa makundi maalum wa asilia, kilichofanyika mwaka uliopita. Hili ni jambo bora sana kwani watu asilia tunaendelea kutambulika zaidi.

Ripoti hiyo iliyozinduliwa ya taarifa ya Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kuhusu utafiti wa Hali ya Haki za watu wenye kuishi maisha asilia Tanzania, imeweza kuangalia mambo mbalimbali ikiwemo suala la haki ya kuishi, Utawala bora na namna ya jamii hizo zinapotokea katika maeneo yao hapa nchini.

Barua ya Shigongo kwa kwa watumishi wa umma

Nawasalimuni nyote katika jina la nchi yetu nzuri Tanzania, Jina ambalo huko nyuma sote tuliliimba “Tazama ramani utaona nchi nzuri, yenye mito na mabonde mengi ya nafaka…nchi hiyo mashuhuri huitwa Tanzaniaaa!” Hakika wimbo huu vijana wengi siku hizi wanashindwa kuuimba, kwa nini? Uzuri wa taifa lao haupo tena, umepotezwa na baadhi yenu watumishi wa umma wasio na uadilifu. 

Sio siri vijana wetu kwa muda mrefu wameshindwa kujivunia taifa lao, wameshindwa kuongea mbele za watu kwa sauti kubwa kwamba wao ni Watanzania, uzuri wa taifa lao na sifa nzuri ya nchi yao imeharibiwa na vitendo kama ufisadi uliokithiri ambao umesababisha wachache katika taifa kunufaika huku wengi wakiteseka. 

Ndugu zangu watumishi wa umma, Ni kwa kupitia jina la nchi hii ndiyo leo nawaandikieni, kuwakumbusha juu ya wajibu wenu ambao kwa muda mrefu sana umekuwa hautimizwi ipasavyo! Kwanza kabisa niseme wazi kwamba nayafahamu mateso yenu, nayafahamu mahangaiko yenu ya maisha magumu, ambayo wakati mwingine yamefanya uaminifu wenu kutikiswa. Pamoja na hayo yote nasema hakuna jambo hata moja linalohalalisha kwenu ninyi kupoteza vigezo vitano muhimu vya utumishi wa umma ambavyo ni; 

1.UADILIFU 
2.UAMINIFU 
3.KUSEMA KWELI DAIMA 
4.UZALENDO NA DHAMIRA 
5.HOFU YA MUNGU. 

Yeyote kati yenu aliyehalalisha kuondoka kwa vitu vitano nilivyovitaja hapo juu kwa sababu ya aidha kipato kidogo anachokipata serikalini, akavunjika moyo na kuacha kuwatumikia wananchi, ama akachagua kuendeleza rushwa na kukosa uzalendo, huyu hatufai kuwa mtumishi wa umma. 

Kwa muda mrefu mmekuwa mkilalamikiwa, mkinung’unikiwa na wananchi kwa sababu ya utendaji mbovu unaosababishwa na kukosekana kwa mambo matano niliyoyataja hapo juu, kwa kweli ilionekana kana kwamba uadilifu katika taifa hili hauwezekani tena, vivyo hivyo uaminifu, kusema kweli, uzalendo na hofu ya Mungu vilitoweka. 

Uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, 2015 na kumwingiza madarakani rais ambaye hawezi kumaliza hotuba yake bila kusema “TUNAMTANGULIZA MUNGU MBELE” Dk. John Pombe Joseph Magufuli umerejesha tena imani ya Watanzania kwamba, kumbe utumishi wa umma uliotukuka unawezekana, yote haya yamefanyika ndani ya siku chini ya arobaini tangu aingie madarakani! 

Kwa matendo yake hayo, nimesikia kwa masikio yangu watu waliompinga Rais Dk. Magufuli wakati wa kampeni wakijuta na kusema: “Laiti ningejua ningempa kura yangu!” haya yanatokea ndani ya siku chini ya hamsini tangu rais huyu aingie madarakani, upepo umebadilika, utumishi wa umma uliowekwa madarakani na watu kwa ajili ya watu kumbe unawezekana. 

Ule msemo wa wazungu usemao “Once you shake the top, you have shaken the bottom” yaani ukishatikisa juu, tayari utakuwa umetikisa na chini, sasa umedhihirika kwamba ni kweli. Tanzania inakimbia mbio, kuanzia serikalini mpaka kwenye sekta binafsi, adui uvivu ameanza kupotea kwa sababu tu raia aliyeingia madarakani sio mvivu. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu nimeanza kusikiliza taarifa za habari na kusikia habari za kamatakamata, fukuzafukuza, kila kona ya nchi. 

kila kiongozi, kila mtendaji sasa anajaribu kutimiza wajibu wake, yote haya kwa sababu amebadilishwa mtu mmoja tu juu ambaye kauli mbio yake ni “HAPA KAZI TU!” Ndugu zangu Watumishi wa Umma, Nawaandikieni barua hii kuwakumbusha kwamba ile kauli yenu ya kusema “huu ni moto wa mabua” naomba muiache, anayesema hivyo hamfahamu vizuri rais wetu, kwa wanaomfahamu hawawezi hata siku moja kutoa kauli hiyo, haigizi, haya ndiyo maisha yake, ni kama mapafu ambavyo kazi yake ni kupumua, ndiyo ilivyo kwa Rais Dk. John Pombe Magufuli. 

Ndugu zangu, Nawasihi mfanye kazi, timizeni wajibu wenu mliopangiwa kwa faida ya taifa hili, ambaye hatayasikia maneno haya, hakika ajiandae kukumbuka ninachokisema kwani mfumo utamtema! Ni wakati wa kuchapa kazi, si wa kuchati kwenye mitandao ya jamii saa ya kazi. 

Tukifanya jambo hili kwa pamoja, ninawahakikishieni taifa letu litasonga mbele kutoka hapa tulipo kwenda tunakotakiwa kwenda, rais wetu ni MUADILIFU, ndivyo itakavyokuwa kwa Makamu wake wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, serikali nzima na hatimaye vijijini, vivyo hivyo katika uchapakazi, kama rais wetu si mvivu, wavivu wote watang’oka, watake wasitake. 

Matarajio yangu ni kwamba kama watumishi wa umma mtatimiza vyema wajibu wenu, mtafanya kazi kwa uadilifu, uaminifu na uzalendo wa hali ya juu, lazima kipato cha taifa letu kitaongezeka na maisha yenu yataboreshwa na rais huyu huyu tuliyemweka madarakani. 

Lakini niwasihi msipoteze hali yenu ya kujiamini kwa kusema “Rais ni mkali mno” matokeo yake mkawa ni watu wa kutekeleza mambo kwa nidhamu ya woga, taifa la watu wenye aina hii ya nidhamu, ambao hutekeleza mambo yao kwa kutaka tu kumfurahisha mkuu huwa halisongi mbele, matokeo yake huzaa hata uonevu kwa sababu tu mtu alikuwa anataka aonekane anafanya kazi. 

Sidhani rais wetu ni mtu wa aina hii, bali ni mtu anayependa kufanya kazi na watu wanaojiamini na wachapakazi na atakuwa tayari kujenga jamii ya watu wenye kujiamini si wanaotetemeka ovyo kila wanapokutana naye wakimpa ushauri anaopenda kuusikia, si ule anaotakiwa kuusikia hata kama hautamfurahisha. 

Nimeyasema haya kwa sababu msipokuwa makini wale mlioko madarakani, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi nk. Mtajikuta mkionea watu au kuwatoa watu sadaka kwa sababu tu mnataka kumfurahisha mkuu au muonekane mnafanya kazi na baadaye kupanda vyeo kwa gharama za maisha ya watu wengine. 

Sitaki kusema mengi siku ya leo, kwa haya machache niliyoyasema nawatakieni utendaji mwema wa kazi katika Awamu hii ya tano ya HAPA KAZI TU! Tendeni kazi zenu kwa kujiamini na uadilifu wa hali ya juu, nawahikikisheni awamu hii ya tano itabadilisha maisha yenu, kama anavyosema mwenyewe Rais Magufuli, tumuombee kwa Mungu atimize ndoto yake yakutufikisha kwenye nchi ya ahadi.

 Ahsanteni.  

NUKUU WASALAAM  
Eric Shigongo James

JAJI MKUU WA TANZANIA MHE. OTHMAN CHANDE ATOA SOMO KWA WAANDISHI WA HABARI

Wednesday, November 25, 2015

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande (kushoto) na Meneja wa Maadili wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Allan Lawa (kulia) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari za Mahakama yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania leo jijini Dar es salaam.

Na. Aron Msigwa –MAELEZO.

Waandishi wa habari nchini wametakiwa kuzingatia weledi wa taaluma zao wanapoandika habari za Mahakama ili kuepuka kuandika habari zinazowatia hatiani watuhumiwa na kushindwa kutofautisha kati ya  mshitakiwa na mtuhumiwa pamoja na haki zake.

Akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa Habari za Mahakama leo jijini Dar es Salaam, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande  amesema waandishi wa habari  wanalojukumu la kuwapatia wananchi taarifa sahihi kuhusu masuala yanayowahusu na kuepuka uandishi wa habari zenye kuhukumu.

Amesema  kisheria mtuhumiwa huwa hana hatia mpaka itakapothibitishwa na mahakama kuwa ametenda kosa na kuongeza kuwa kukosekana kwa weledi katika uandishi wa habari za mahakama  huleta mkanganyiko  miongoni mwa jamii  kuhusu ukweli na kuondoa imani ya watu kwa mahakama.

Ameongeza kuwa baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa Vikitoa  habari zisizo mpatia mtu  fursa na haki ya kujibu tuhuma huku vingine vikitoa taarifa nusunusu na kushindwa kuwa na mwendelezo wa habari za mashauri mbalimbali mahakamani.

Mhe.Chande ameeleza kuwa waandishi wamejikita katika uandishi wa taarifa zenye mvuto kwa jamii na kusahau nyingine walizo anza nazo jambo  linalosababisha wananchi kuachwa  njia panda bila kupata taarifa za kina kuhusu mwisho wa mambo yanayoanzishwa.

" Mimi sitaki kuingilia utendaji wa kazi zenu za kila siku ila nachotaka kusema ni kuweka msisitizo wa utoaji wa habari za mashauri mbalimbali mnayoanza kuyaripoti kwa mwendelezo ili msiwachanganye wananchi" Amesisitiza.

Amewataka waandishi wa habari kuandika habari sahihi na kuepuka upendeleo na maslahi binafsi ili kulinda taaluma na imani katika jamii juu ya utendaji wa vyombo vya habari.

Mhe. Chande ametoa wito kwa waandishi wa habari kuepuka uandishi wa habari zilizojaa chuki zinazoweza kuleta mgawanyiko katika jamii na kusisitiza habari za kuisaidia jamii kukabiliana na changamoto mbalimbali.

Kuhusu Mahakama amesema itaendelea kuboresha huduma na miundombinu yake katika maeneo yasiyofikiwa ili kuendelea kutoa haki kwa wakati pia  kushirikiana na waandishi wa habari wa ndani ili kuimarisha utendaji wao.

Aidha amevipongeza vyombo vya habari kwa ukomavu  viliouonyesha wakati wa utoaji wa taarifa za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Kwa upande wake Rais wa Baraza la Habari Tanzania Mhe. Jaji Mstaafu Mhe.Thomas Mihayo  akizungumza kwa niaba ya Baraza hilo ametoa wito kwa waandishi wa habari kuzingatia weledi katika uandishi wa habari za mahakama ili kuepusha madhara katika jamii.

Amewataka waandishi kujikita zaidi katika uandishi wa habari zenye uhakika kuliko kuwa na taarifa zenye mlengo wa kuuza gazeti.

Amesema kuwepo kwa mafunzo hayo ambayo yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania ni ishara nzuri ya uboreshaji wa taaluma ya habari hasa uongezaji wa ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya  kimahakama hapa nchini.

Amewataka wanahabari kujifunza na kufuatilia miongozo na kufuatilia taarifa mbalimbali zinazoweza kuboresha uandishi wao kwa kupata maneno sahihi ya kimahakama.Amesema Semina hiyo itawasaidia waandishi wa habari kujenga weledi katika uandishi wa habari za mahakama.

Ametoa tahadhari kwa waandishi kuepuka uandishi wa habari zenye uchochezi ili kuepuka kushtakiwa na jamii, kuepuka lugha za kishabiki na upendeleo.

Naye Meneja wa Maadili wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Allan Lawa akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo amewataka kuepuka kuandika habari zinaonyesha upendeleo na  kubainisha kuwa kuwa ipo haja kwa vyombo vya habari kutenga maeneo madawati ya habari hizo

Baraza la Mawaziri: Magufuli Kefyeka Nusu ya Wizara za Kikwete Hizi ndizo wizara za serikali yake

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, anatarajiwa kuzifuta wizara 15 kati ya zilizopo sasa na kubaki na baraza dogo litakalokuwa na wachapakazi makini ili kutimiza dhamira yake ya kubana matumizi na kuinua maisha ya Watanzania.
Kadhalika, inaelezwa kuwa Dk. Magufuli aliyeahidi kuleta mabadiliko ya kweli wakati akiomba kura kwa Watanzania kabla ya kuibuka na ushindi wa asilimia 58.46 dhidi ya wapinzani wake katika uchaguzi mkuu Oktoba 25, sasa yuko mbioni kutangaza baraza lake la mawaziri litakalokuwa na wizara 15, idadi inayofanana kwa kiasi kikubwa na ile ya Baraza la Mawaziri la miaka ya 1980 lililoundwa na Rais wa Awamu ya Kwanza, Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere. 
Serikali ya awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete, ilimaliza muda wake Novemba 5, 2015  ikiwa na Wizara 30. Kadhalika, alipoingia kwa mara ya kwanza mwaka 2005, Rais Kikwete alikuwa na serikali kubwa yenye mawaziri na naibu wao zaidi ya 60.   
Kufikia leo, Rais Magufuli aliyeapishwa Novemba 5, mwaka 2015, tayari ameshamteua Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa, kuwa Waziri Mkuu wa serikali yake ya awamu ya tano na Ijumaa iliyopita alizindua rasmi Bunge la 11.
Chanzo kimoja cha uhakika kimedokeza jana kuwa hivi sasa, tayari Rais Magufuli kwa kushirikiana na wasaidizi wake, ameshakamilisha sehemu kubwa ya mchakato wa kuunda baraza lake la mawaziri na kwamba, kinachosubiriwa sasa ni kulitangaza wakati wowote kuanzia sasa.
Chanzo hicho kilidai kuwa Dk. Magufuli ambaye amejichimbia mjini Dodoma tangu mwishoni mwa wiki iliyopita, anatarajiwa kutangaza baraza lake dogo la mawaziri wakati wowote kuanzia leo.
“Halitakuwa sawa na hili alilomaliza nalo Rais Kikwete… na wala halitakuwa na watu wengi kama lile aliloingia nalo kwa mara ya kwanza Rais Kikwete mwaka 2005. Ni baraza dogo tu na wizara kadhaa hazitakuwapo,” kilisema chanzo hicho.
Kwa mujibu wa ibara ya 55 (1) ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mawaziri wanakuwa wajumbe wa Baraza la Mawaziri na pia kwa mujibu wa ibara ya 54, mawaziri huteuliwa na rais baada ya kushauriana na Waziri Mkuu. 
“Kuna mambo madogo bado hayajakamilika… baada ya hapo Mheshimiwa Rais atalitangaza Baraza la Mawaziri siku yoyote kuanzia leo. Kimsingi mkakati wake ni kuwa na baraza dogo lenye wizara 15,” kilieleza chanzo hicho.
Aidha, ilielezwa zaidi kuwa sura kadhaa katika baraza hilo dogo zitakuwa mpya na kwamba, mawaziri waliokuwamo katika serikali ya awamu ya nne wana nafasi ndogo ya kuteuliwa katika baraza hilo.
“Kwa kiasi fulani Baraza hili jipya linafanana na lile la Serikali ya Mwalimu Nyerere miaka ya 1980… lina wizara chache sana, zenye lengo la kubana matumizi ya serikali lakini likiwa na uhakika wa kuchapa kazi usiku na mchana ili kutimiza lengo la Rais Magufuli katika kuwaletea maisha bora Watanzania,” chanzo kiliongeza.
Kumbukumbu zinaonyesha kuwa miaka ya 1980, Mwalimu Nyerere alikuwa na serikali yenye wizara 15; ambazo ni Wizara ya Elimu; Wizara ya Mipango; Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; Wizara ya Mambo ya Ndani; Wizara ya Ujenzi; Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi na Wizara ya Kazi na Ustawi wa Jamii.
Wizara nyingine wakati huo ni Wizara ya Habari na Utamaduni; Wizara ya Afya; Wizara ya Nishati, Madini na Maji; Wizara ya Sheria;  Wizara ya Viwanda na Biashara; Wizara ya Kilimo na Wizara ya Fedha.

WAKENYA WANAVYOMZUNGUMZIA RAIS MAGUFULI


Na Francis Godwin
Unajua nini mtu wangu una kila sababu ya kujivunia kuwa Tanzania wakati na muda kama huu kwani kasi ya Rais wetu Dk. John Pombe Magufuli inaweka headlines kubwa sana kwa nchi za jirani na si kwa Watanzania pekee!
Nimetembelea mtandao wa kijamii wa Twitter na nimekutana na tweets za Wakenya juu ya Rais Dk. John Pombe Magufuli na kwenye kuzisoma tweets zao nimegundua sifa za Rais Magufuli na maamuzi yake ya kazi toka ameshika rungu la Tanzania zimewafikia.
Wengi wamemsifia na wengine wameandika wakiomba Mungu awape Rais kama Magufuli….. tweets nyingine unaweza kuzisoma kwenye hii post.



Kwa kipindi kifupi alichoingia madarakani, Rais Dk. John Magufuli amefanya mambo kadhaa ambayo yamewaridhisha na kuwapa moyo Watanzania, mambo hayo ni kama…
1. Ziara yake ya kushtukiza kwenye hospitali ya Taifa Muhimbili  ilivumbua vitu vingi na kumpelekea Rais Magufuli kufuta bodi ya Wakurugenzi wa hospitali hiyo pamoja na kumuondoa Kaimu Mkurugenzi wake, Dk. Hussein Kidanto.
2. Kufuta safari za viongozi kwenda nchi za nje ili kupunguza matumizi makubwa ya pesa za Serikali.
3. Alielekeza shilingi milion 225 zilizochangwa kwa ajili ya kugharamia hafla ya Pongezi za Wabunge Dodoma kutumika kununua vitanda vya hospitali na shilingi milion 15 tu ndio zitumike kwaajili ya sherehe hiyo.
4. Jumatatu ya tarehe 23 November 2015, Rais Dk. John Magufuli alitangaza kufuta kwa sikukuu ya Uhuru December 9 na kuagiza fedha za maandalizi ya sikukuu hiyo zitumike kutatua matatizo mengine pia ameagiza siku hiyo itumike kusafisha mazingira ili kupunguza matatizo ya kipindupindu nchini.
Mambo haya machache na makubwa yamewapa faraja kubwa sana Watanzania na kumfanya Rais Magufuli awe topic kubwa kwenye mtandao wa Twitter kwa raia wa Kenya!
Kama kawaida kazi yangu ni kuzinasa zile zote zinazoweka headlines wakati huu na hizi ni baadhi ya#tweets nilizofanikiwa kuzinasa, karibu uzipitie moja baada ya nyingine uone jinsi gani Wakenyawalivyoguswa…

TAMKO LA JUKWAA HURU LA WAZALENDO KUUNGA MKONO HOTUBA YA MAGUFULI

Mwenyekiti wa Jukwaa Huru la Wazalendo Ndugu Salum Ally Hapi akizungumza na waandishi wa habari kwenye hotel ya Travetine ,Magomeni jijini Dar es Salaam, kulia ni Katibu wa Jukwaa hilo Ndugu Mtela Mwampamba.

Ndugu wanahabari,

 Mbele yenu sisi tuliowaita hapa ni Jukwaa Huru la Wazalendo ambalo limeitisha mkutano huu ili kufikisha yale tuliyoyakusudia kuwaeleza umma wa watanzania.

 Sote tunatambua kuwa nchi yetu imetoka katika uchaguzi mkuu ambao umetupatia viongozi wapya wa awamu ya tano ya uongozi wa taifa letu chini ya Dr. John Pombe Joseph Magufuli. Tunapenda kuwapongeza watanzania wote kwa uchaguzi wa amani na utulivu. Aidha kwakua ndio mara yetu ya kwanza kuzungumza nanyi tunapenda kuwapongeza wanahabari wote kwa kazi nzuri ambayo mmekua mkiifanya kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu nchini. Tunawashukuru sana.


 Mkutano wetu huu umebeba madhumuni makubwa mawili.

 Kwanza ni kumpongeza Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa  hotuba yake aliyoitoa Bungeni siku ya ufunguzi wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo tarehe 19/11/2015. 

Tunaiunga mkono Hotuba yake ambayo kwa kweli ilikuwa imebeba Uzalendo, Ujasiri, dira ya kweli ya maendeleo ya taifa letu na muuelekeo mpya wa Serikali ya awamu ya tano. Mambo yote aliyozungumzia Mh. Rais yamebeba maslahi mapana ya nchi yetu na yanalenga kuijenga Tanzania mpya ambayo waasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Amani Karume walikusudia kuijenga.


 Pili, pamoja na mambo mengi yaliyogusiwa na hotuba ya Mh. Rais, eneo la kubana matumizi na kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kwa Serikali ni  moja katika mambo ambayo Jukwaa hili limeamua kuyaunga mkono kwa vitendo. Mh. Rais alitoa mchanganuo wa eneo moja tu la safari za nje na jinsi lilivyo ligharimu Taifa mabilioni ya shilingi na kuahidi kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wake itajikita katika kupunguza matumizi yasiyo ya lazima.


 Aidha Mh. Rais ameanza kutekeleza kwa vitendo ahadi yake hiyo ya kupunguza matumizi yote yasiyo ya lazima Serikalini, ikiwemo hafla, warsha, makongamano na safari za nje. 


 Jukwaa Huru la Wazalendo, linatambua kuwa kwa miaka kadhaa mbunge wa Kigoma Mjini Mh. Zitto Kabwe amekuwa na msimamo wa kutokupokea posho za kitako tangu akiwa mbunge wa Kigoma Kaskazini katika Bunge la 10. Pamoja na mh. Zitto, Jukwaa pia limepokea taarifa za baadhi ya wabunge wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walioamua kuunga mkono juhudi za Mh. Rais za kupunguza matumizi yasiyo ya lazima serikalini kwa kukataa hadharani kupokea posho ya kitako ya mbunge (sitting allowance).


 Mnamo tarehe 23/11/2015, mbunge wa Singida Magharibi (CCM) Mh. Elibariki Imanuel Kingu alimwandikia barua Katibu wa Bunge akieleza msimamo wake wa kukataa kulipwa posho ya kitako ya Bunge (sitting allowance) katika kipindi chote cha miaka mitano (2015 -  2020). Huyu anakuwa ni mbunge wa pili baada ya Mh. Zitto Kabwe kutoka hadharani na kukataa posho ambazo msingi wake ni unyonyaji wa wanyonge na ubadhirifu wa kodi za wananchi. 

 Jukwaa linapenda kumpongeza Mh. Kingu Mbunge kwa ujasiri wake na Uzalendo kwa Taifa lake, uliomfanya kuunga mkono juhudi za Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa vitendo. 

 Jukwaa linatambua ya kwamba, mapambano ambayo Mh. Kingu Mbunge ameyaanzisha ni makubwa, magumu na yanahitaji kuungwa mkono na watanzania wote wanaoipenda nchi yao bila kujali itikadi za vyama. Tunafahamu, wapo baadhi ya wabunge wabinafsi na wasio na huruma na wanyonge wa Taifa letu ambao hawajafurahishwa na hatua hii ya wabunge kama Zitto na Kingu ya kukataa posho ya kitako. Baadhi ya wabunge wameanza kumpigia simu na kumtumia jumbe (sms) za vitisho mh. Elibariki Kingu (MB) na wengine wakibeza kuwa anatafuta cheo.


 Jukwaa linalaani hatua za wabunge hao wanaopinga nia njema ya Mh. Elibariki Kingu na Mh. Zitto Kabwe kwa uamuzi wao wa kukataa posho za kinyonyaji na hivyo basi, Jukwaa linawaomba wananchi wote majimboni, kuwataka wabunge wao waliowachagua kueleza misimamo yao hadharani juu ya kuunga mkono hatua ya kukataa posho kama njia ya kupunguza matumizi ya Serikali yasiyo ya lazima.


 Jukwaa linafahamu ya kwamba, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiye mwenye mamlaka ya mwisho ya kuidhinisha masharti ya kazi za kibunge na stahiki wanazopaswa kulipwa katika kazi hiyo.Kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, tunamuomba na kumshauri Mh. Rais John Pombe Magufuli atakapokuwa anaidhinisha masharti na stahiki hizo, atusaidie kuifuta kabisa posho ya kitako ya wabunge (sitting allowance). 

 Aidha, Jukwaa linamuomba mh. Rais kuzipitia na kutoa agizo la kufutwa kwa posho zote zisizo za lazima zinazolipwa kwa watumishi wa umma wa kada mbalimbali yakiwemo mashirika ya umma.


 Jukwaa letu linatoa wito kwa wabunge wote bila kujali vyama vyao, kuungana na Mh. Kingu(MB) na Mh. Zitto(MB) katika kukataa malipo ya posho ya kitako ili kupunguza mzigo mkubwa ambao Serikali inaubeba kuhudumia wabunge. Fedha hizi ni vyema zielekezwe katika kutatua kero za wananchi vijijini kama vile ukosefu wa maji, madawati, vitanda vya Hospitali n.k.


 Tunasisitiza kwamba, Ubunge ni Utumishi,na wala sio Utukufu. Kazi ya Mbunge ni kuwawakilisha wananchi wake na si kuwanyonya. Tufike mahali kama Taifa tuwe na nidhamu ya matumizi ya kodi za wananchi na mgawanyo sawa wa keki ya Taifa. Kuendelea kulipana posho hizo ni ishara ya unyonyaji, dhuluma na kuongeza pengo kati ya wenye nacho na wasionacho nchini. Jambo hili linakuza chuki na hasira miongoni mwa wananchi wa hali ya kawaida dhidi ya viongozi wao na serikali kwa ujumla.


 Tunawaahidi kuwa Jukwaa litaendeleza harakati (movement) na vuguvugu hili kwa kuanzia na Bunge kwasababu ndio wawakilishi wa wananchi. Tutaendelea kupaza sauti zetu ili wabunge wengi zaidi Wazalendo wajitokeze na kukataaa posho hizi. Tunajua kuwa wapo miongoni mwao wabunge wazalendo ambao wataguswa na wito huu na kuuunga mkono hadharani. 

 Aidha tutaendelea kuwasemea kwa wananchi wabunge ambao bado hawataki kukataa posho hizi bila kujali vyama vyao. Tunawaomba wananchi kote nchini kutuunga mkono katika harakati hizi ili tuweze kuokoa mabilioni ya shilingi yanayopotea kila Bunge linapokaa Dodoma kupitia posho ya kitako (sitting allowance).

Tutaandaa maandamano nchi nzima ya kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi kuwashinikiza wabunge kukataa posho hizi. Makongamano na mdahalo mbalimbali itaandaliwa na jukwaa ili kujenga uelewa wa pamoja wa wananchi na kuwa na sauti moja katika kupinga posho za wabunge, watumishi wa serikali na mashirika ya umma. Haya yatafanyika katika kufikia kusudio letu la kumuunga mkono Mheshimiwa Rais katika hatua yake ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kwa Serikali. 


Hatutaogopa wala kutishwa na yeyote katika kutekeleza jukumu hili zito. 


 Ahsanteni sana.

 ALLY SALUM HAPI  - MWENYEKITI
 MTELA MWAMPAMBA  - KATIBU
kutoka michuzi
 

Most Reading

Eckros Computer Lap 1

Eckros Computer Lap 1

About ETC College

Eckros Tourism College (ETC) started admitting the first intake of students in January 2013. The college falls under tertiary higher education and training as stipulated in education and training policy of 1995.
Also the college administer Distance Learning Programmes, Evening classes, weekend classes, study tours and researchs programmes
Admission Process
New admission into the College is effected twice a year in January-July and July-December.

WALIO PITIA BLOG YETU